WATOTO WALIOPATA AJALI WAKITOKEA KANISANI WAPOKEA MALIPO KUTOKA BUMACO INSURANCE CO. LTD

WATOTO WALIOPATA AJALI WAKITOKEA KANISANI WAPOKEA MALIPO KUTOKA BUMACO INSURANCE CO. LTD

  • Date 06-06-2025

Wazazi wa Watoto sita waliopata ajali baada ya kugongwa na gari aina ya Haice wakitokea kanisani, ambapo mmoja wao alifariki dunia, wamekabidhiwa malipo ya gharama za matibabu na mazishi kutoka kwa kampuni ya bima ya Bumaco Insurance.

Tukio hilo lililotokea mapema mwaka huu limeacha alama ya huzuni kwa jamii, hasa kwa familia iliyompoteza mtoto wao.

Hata hivyo, kampuni hiyo ya bima imejitokeza kusaidia familia hizo kwa kuzingatia masharti ya bima yaliyokuwepo kwa chombo kilichohusika katika ajali hiyo.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi malipo hayo kwa wazazi wa watoto hao, Meneja wa Mauzo wa Bumaco Insurance mkoa wa Kilimanjaro, Gasto Mrema, amesisitiza umuhimu wa kuwa na bima, akisema ni kinga muhimu wakati wa majanga.

“Bima si anasa bali ni hitaji. Hakuna ajuaye kesho, hivyo ni vema kila mmiliki wa chombo cha moto kuhakikisha anakata bima ili kusaidia wakati wa dharura kama hizi,” alisema Mrema.

Hata hivyo amewashauri wamiliki wa vyombo vya moto kuhakikisha kuwa wanakata bima kwa ajili ya vyombo vyao ili kuwalinda wanapopatwa na majanga ya ajali huku akiwasihi madereva kutokukubali kutembea na chombo cha moto barabarani kisichokuwa na bima.

Kwa upande wao, baadhi ya wazazi wa watoto waliopata ajali hiyo wameishukuru kampuni ya bima Bumaco Insurance kwa msaada waliopokea, wakisema umeleta faraja katika kipindi kigumu walichopitia.

“Tumepitia maumivu makubwa, lakini msaada huu umetufuta machozi, tunawashukuru Bumaco kwa moyo huu wa huruma, na tunatarajia waendelee kusaidia wengine watakapopatwa na majanga kama haya,” alisema mmoja wa wazazi.

Ajali hiyo iliibua mjadala mpana kuhusu umuhimu wa bima za magari, huku wadau wa usalama barabarani wakihimiza elimu zaidi kwa wananchi kuhusu sheria na haki zao katika mifumo ya bima.